Zaburi 129
Maombi Dhidi Ya Adui Za Israeli 
 
Wimbo wa kwenda juu. 
 
1 Wamenionea mno tangu ujana wangu;  
Israeli na aseme sasa:   
2 wamenionea mno tangu ujana wangu,  
lakini bado hawajanishinda.   
3 Wakulima wamelima mgongo wangu,  
na kufanya mifereji yao mirefu.   
4 Lakini Bwana ni mwenye haki;  
amenifungua toka kamba za waovu.   
   
 
5 Wale wote waichukiao Sayuni  
na warudishwe nyuma kwa aibu.   
6 Wawe kama majani juu ya paa,  
ambayo hunyauka kabla hayajakua;   
7 kwa hayo mvunaji hawezi kujaza vitanga vyake,  
wala akusanyaye kujaza mikono yake.   
8 Wale wapitao karibu na wasiseme,  
“Baraka ya Bwana iwe juu yako;  
tunakubariki katika jina la Bwana.”