15
Agano La Mungu Na Abramu
Baada ya jambo hili, neno la Bwana likamjia Abramu katika maono:
“Usiogope, Abramu.
Mimi ni ngao yako,
na thawabu yako kubwa sana.”
Lakini Abramu akasema, “Ee Bwana Mwenyezi, utanipa nini na mimi sina hata mtoto na atakayerithi nyumba yangu ni huyu Eliezeri Mdameski?” Abramu akasema, “Hukunipa watoto, hivyo mtumishi katika nyumba yangu ndiye atakuwa mrithi wangu.”
Ndipo neno la Bwana lilipomjia: “Mtu huyu hatakuwa mrithi wako, bali mwana atakayetoka katika viuno vyako mwenyewe ndiye atakayekuwa mrithi wako.” Akamtoa nje na kusema, “Tazama juu kuelekea mbinguni na uhesabu nyota, kama hakika utaweza kuzihesabu.” Ndipo akamwambia, “Hivyo ndivyo uzao wako utakavyokuwa.”
Abramu akamwamini Bwana, naye kwake hili likahesabiwa kuwa haki.
Pia akamwambia, “Mimi ndimi Bwana, niliyekutoa toka Uru ya Wakaldayo nikupe nchi hii uimiliki.”
Lakini Abramu akasema, “Ee Bwana Mwenyezi, nitawezaje kujua kwamba nitapata kuimiliki?”
Ndipo Bwana akamwambia, “Niletee mtamba wa ngʼombe, mbuzi na kondoo dume, kila mmoja wa miaka mitatu, pamoja na hua na kinda la njiwa.”
10 Abramu akamletea hivi vyote, akampasua kila mnyama vipande viwili, akavipanga kila kimoja kuelekea mwenzake, lakini hata hivyo ndege, hakuwapasua vipande viwili. 11 Kisha ndege walao nyama wakatua juu ya mizoga, lakini Abramu akawafukuza.
12 Wakati jua lilipokuwa linatua, Abramu akashikwa na usingizi mzito, giza nene na la kutisha likaja juu yake. 13 Kisha Bwana akamwambia, “Ujue hakika kwamba wazao wako watakuwa wageni kwenye nchi ambayo si yao, nao watafanywa watumwa na kuteswa kwa miaka mia nne. 14 Lakini nitaliadhibu taifa lile watakalolitumikia kama watumwa, na baadaye watatoka huko na mali nyingi. 15 Wewe, hata hivyo utakwenda kwa baba zako kwa amani na kuzikwa katika uzee mwema. 16 Katika kizazi cha nne wazao wako watarudi hapa, kwa maana dhambi ya Waamori bado haijafikia kipimo kilichojaa.”
17 Wakati jua lilipokuwa limezama na giza limeingia, tanuru la moshi na mwali wa moto unaowaka vikatokea na kupita kati ya vile vipande vya nyama. 18 Siku hiyo Bwana akafanya Agano na Abramu, na kumwambia, “Nitawapa wazao wako nchi hii, kuanzia Kijito cha Misri* hadi mto ule mkubwa, Frati, 19 yaani nchi ya Wakeni, Wakenizi, Wakadmoni, 20 Wahiti, Waperizi, Warefai, 21 Waamori, Wakanaani, Wagirgashi na Wayebusi.”
* 15:18 Kijito cha Misri hapa ina maana Wadi-el-Arish kwenye mpaka wa kusini wa Yuda.