28
Utakaposikiliza kwa makini sauti ya Yahwe Mungu wako ili kwamba ushikilie amri zake zote ambazo nakuamuru leo, Yahwe Mungu wako atakuweka juu ya mataifa yote ya ulimwengu. Baraka hizi zote zitakuja kwako na kukupita, kama utasikiliza sauti ya Yahwe Mungu wako. Utabarikiwa ndani ya mji, na utabarikiwa shambani. Matunda ya mwili wako yatabarikiwa, na matunda ya ardhi yako, na matunda ya wanyama wako, ongezeko la ng’ombe wako, na wachanga wa mifugo wako. Kitabarikiwa kikapu chako na chombo cha kukandia. Utabarikiwa utakaporudi ndani, na utabarikiwa utakapotoka nje. Yahwe atasababisha maadui zako wanaoinuka dhidi yako kupigwa chini mbele yako; watajitokeza dhidi yako kwa njia moja lakini watakimbia mbele zako kwa njia saba. Yahwe ataamuru baraka kuja kwako katika maghala yako na katika kila unapoweka mkono wako; atakubariki katika nchi anayokupatia. Yahwe atawaimarisha kama watu waliotengwa kwa ajili yake, kama alivyoapa kwenu, iwapo mtashikilia amri za Yahwe Mungu wenu, na kutembea katika njia zake. 10 Watu wote wa ulimwengu wataona ya kwamba mmeitwa kwa jina la Yahwe, nao watawaogopa. 11 Yahwe atakufanya kuwa na mafanikio sana katika matunda ya mwili wako, katika matunda ya ng’ombe zako, katika matunda ya ardhi yako, katika nchi aliyoapa kwa mababu zako kuwapatia. 12 Yahwe atafungua kwako ghala lake la mbingu kuruhusu mvua juu ya ardhi katika muda sahihi, na kubariki kazi zote za mikono yako; utakopesha kwa mataifa mengi, lakini wewe hautakopa. 13 Yahwe atakufanya kuwa kichwa, na sio mkia; utakuwa juu tu, na hautakuwa chini, iwapo utaisikiliza amri za Yahwe Mungu wako ambazo ninakuamuru leo, ili kuzishikilia na kuzitenda, 14 na usipogeuka kinyume na maneno yoyote ninayokuamuru leo, kulia kwako wala kushoto kwako, na kufuata miungu mingine na kuwatumikia. 15 Lakini usiposikiliza sauti ya Yahwe Mungu wako, na kushikilia amri zake zote na sheria zake ninazokuamuru leo, basi laana hizi zote zitakuja kwako na kukupita. 16 Utalaaniwa utakapokuwa mjini, na utalaaniwa utakapokuwa shambani. 17 Kitalaaniwa kikapu chako na chombo chako cha kukandia. 18 Litalaaniwa tunda la mwili wako, tunda la ardhi yako, ongezeko la ng’ombe wako, na wachanga wa mifugo. 19 Utalaaniwa utakaporudi, na utalaaniwa utokapo. 20 Yahwe atatuma laana juu yako, kuchanganyikiwa, na shutuma katika kila jambo uwekalo mikono yako, hadi utakapoangamizwa, na hadi utakapotoweka haraka kwa sababu ya matendo yako maovu ambayo utakuwa umenitelekeza mimi. 21 Yahwe atafanya pigo likung’ang’anie mpaka kukuangamiza kutoka katika nchi utakayoenda kumiliki. 22 Yahwe atakushambulia kwa magonjwa ya kuambukiza, kwa homa, kwa uvimbe, na kwa kiangazi na jua kali, na kwa upepo mkali na ukungu. Hivi vitakufukuza hadi uangamie. 23 Mbingu zilizo juu ya vichwa vyenu zitakuwa shaba, na ardhi chini yenu itakuwa chuma. 24 Yahwe atafanya mvua ya ardhi yako kuwa unga na vumbi, kutoka mbinguni vitashuka kwako, hadi utakapoangamizwa. 25 Yahwe atakusababishia upigwe mbele ya maadui zako; utawafuata kwa njia moja dhidi yao lakini utakimbia mbele zao kwa njia saba. Utapelekwa huku na kule miongoni mwa falme za nchi. 26 Mzoga wako utakuwa chakula kwa ndege wote wa angani na kwa wanyama wa ulimwengu; hakutakuwa na mtu wa kuwatisha. 27 Yahwe atawashambulia na majipu ya Misri na vidonda, kiseyeye na mwasho ambazo hautapona. 28 Yahwe atakushambulia kwa ukichaa, kwa upofu, pamoja na kuchanganyikiwa kwa akili. 29 Utapapasa papasa mchana kama kipofu apapasavyo usiku, na hautafanikiwa katika njia zako; daima utakandamizwa na kuporwa, na hakutakuwa na mtu wa kukuokoa. 30 Utamchumbia mwanamke, lakini mwanamume mwingine atamkamata na kumbaka. Utajenga nyumba lakini hautaishi ndani mwake; utapanda shamba la mizabibu lakini hautafurahia matunda yake. 31 Ng’ombe wako atachinjwa mbele ya macho yako, lakini hautakula nyama yake; punda wako atachukuliwa kwa nguvu mbele yako na hatarejeshwa kwako. Kondoo wako watapewa maadui zako, na hautakuwa na mtu wa kukusaidia. 32 Watoto wa kiume na mabinti zako watapewa kwa watu wengine; macho yako yatawatafuta siku nzima, lakini yatashindwa kwa shauku juu yao. Hakutakuwa na nguvu mikononi mwako. 33 Mavuno ya ardhi yako na ya kazi yako yote – taifa usilolijua litayatafuna; daima utaonewa na kugandamizwa, 34 ili upatwe na wazimu kwa yale utakayoona yakitendeka. 35 Yahwe atakushambulia kwenye magoti na miguu kwa majibu makali ambayo hutaweza kupona, kutoka chini ya miguu yako mpaka juu ya kichwa chako. 36 Yahwe atawachukua pamoja na mfalme ambaye mtakuwa mmemuweka juu yenu kwa taifa ambalo hamjalijua, wala nyie au mababu zenu; kule mtaabudu miungu mingine ya mbao na mawe. 37 Nawe utakuwa chanzo cha kitisho, mithali, na uvumi, miongoni mwa watu wote ambako Yahwe atakupeleka. 38 Utaweka mbegu nyingi shambani, lakini utakusanya mbegu chache, kwa maana nzige itaziangamiza. 39 Utapanda mashamba ya mizabibu na kuyapalilia, lakini hautakunywa divai yoyote, wala hautakusanya matunda yoyote, kwa maana funza watayala. 40 Utakuwa na miti ya mizeituni katika eneo lako, lakini hautajipaka mafuta yoyote juu yako, kwa maana mti wako wa mzeituni utaangusha matunda yake. 41 Utakuwa na wana wa kiume na mabinti, lakini hawatabaki kuwa wako, kwani watachukuliwa mateka. 42 Miti yako yote na matunda ya ardhi yako – nzige watajitwalia. 43 Mgeni aliye miongoni mwako atainuka juu zaidi yako juu na juu; wewe mwenyewe utashuka chini na chini. 44 Atakukopesha, lakini hautamkopesha; atakuwa kichwa, nawe utakuwa mkia. 45 Laana hizi zote zitakujia juu yako na kukuandama na kukupita hadi utakapoangamizwa. Hii itatokea kwa sababu haukuisikia sauti ya Yahwe Mungu wako, ili kushikilia amri na maagizo yake aliyokuamuru. 46 Laana hizi zitakuwa juu yako kama ishara na miujiza, na juu ya uzao wako milele. 47 Kwa sababu hukumuabudu Yahwe Mungu wako kwa shangwe na furaha moyoni mwako ulipokuwa na mafanikio, 48 kwa hiyo utatumikia maadui ambao Yahwe atatuma dhidi yako; utawatumikia katika njaa, katika kiu, katika uchi, na katika umaskini. Ataweka mzigo wa chuma juu ya shingo yako hadi akuangamize. 49 Yahwe ataleta taifa dhidi yako kutoka mbali, kutoka mwisho wa ulimwengu, kama tai arukaye kwa mhanga wake, taifa ambalo lugha yake hauelewi; 50 taifa lenye sura katili ambalo haliheshimu wazee na halionyeshi fadhila kwa wadogo. 51 Watakula wachanga wa ng’ombe wako na matunda ya ardhi yako hadi utakapoangamizwa. Hawatawaachia nafaka, divai mpya, au mafuta, wachanga wa ng’ombe au mifugo yako, hadi watakaposababisha kutoweka kwako. 52 Watawazingira katika malango ya miji yenu, hadi kuta zenu ndefu na imara zitakaposhuka chini ardhini, kuta ambazo mliziamini. Watawazingira ndani ya malango ya miji yenu kotekote katika nchi ambayo Yahwe Mungu wenu amewapatia. 53 Utakula tunda la mwili wako mwenyewe, nyama ya watoto wa kiume na binti zako, ambao Yahwe Mungu wako aliwapatia, katika uvamizi na katika dhiki ambayo adui zako wataweka juu yako. 54 Mwanamume laini na mlegevu miongoni mwenu – atakuwa na wivu kwa kaka yake na kwa mkewe, na kwa watoto wowote waliosalia. 55 Kwa hiyo hatawapatia kati yao nyama ya watoto wake ambayo ataenda kuila, kwa sababu hatabakiwa na chochote katika uvamizi na dhiki ambayo adui yako ataiweka juu yako ndani ya malango yote ya mji wako. 56 Mwanamke laini na mlegevu miongoni mwenu, ambaye hatadiriki kuweka tako la mguu wake ardhini kwa sababu ya ulaini na maringo yake – atakuwa na wivu kwa mume kipenzi wake mwenyewe, kwa mtoto wake wa kiume, na kwa binti yake, 57 na kwa mtoto wake mchanga atakayetoka katikati ya miguu yake, na kwa watoto atakayewazaa. Atawala kwa siri kwa kukosa kitu kingine, katika uvamizi na dhiki ambayo adui yako ataweka juu yako ndani ya malango ya mji wako. 58 Iwapo hautashika maneno yote ya sheria yaliyoandikwa katika kitabu hiki, ili kuheshimu jina hili tukufu na la kutisha, Yahwe Mungu wako, 59 basi Yahwe atafanya mapigo yako kuwa ya kutisha, na yale ya wazao wako; yatakuwa mapigo makuu, ya muda mrefu, na magonjwa makali, ya muda mrefu. 60 Ataleta juu yako mara nyingine magonjwa yote ya Misri ambayo ulikuwa unayaogopa; yatakung’ang’ania. 61 Pia kila gonjwa na pigo ambalo halijaandikwa katika kitabu cha sheria hii, hayo pia Yahwe atayaleta juu yako hadi utakapoangamizwa. 62 Utabaki wachache kwa idadi, ingawa ulikuwa kama nyota wa mbinguni kwa idadi, kwa sababu haukuisikiliza sauti ya Yawhe Mungu wako. 63 Kama vile hapo awali Yawhe alivyofurahia juu yako na kutenda mema, na kuwazidisha, basi atafurahia juu yako kwa kufanya upotee na kwa kukuangamiza. Utang’olewa katika nchi utakayoenda kuimiliki. 64 Yahwe atakusambaza miongoni mwa watu wote kutoka mwisho mmoja wa dunia hadi mwisho mwingine wa dunia; huko utaabudu miungu mingine ambayo hujawajua, wewe wala mababu zako, miungu ya mbao na jiwe. 65 Miongoni mwa mataifa haya hautapata utulivu, na hakutakuwa na pumziko chini ya miguu yako; badala yake, Yahwe atakupatia huko moyo wa kutetemeka, macho yanayofeli na nafsi inayoomboleza. 66 Maisha yako yataning’inia kwa mashaka mbele yako; utaogopa kila usiku na mchana na hutakuwa na uhakika kabisa maishani mwako. 67 Asubuhi utasema, “Natamani ingekuwa jioni! ” na jioni utasema, “Natamani ingekuwa asubuhi! ” kwa sababu ya hofu mioyoni mwenu na vitu ambavyo macho yako italazimu kuona. 68 Yahwe atakuleta Misri mara nyingine kwa meli, kwa njia ambayo nilikuambia, “Hutaiona Misri tena”. Kule utajitoa kuuzwa kwa maadui zako kama watumwa wa kiume na kike, lakini hakutakuwa na mtu wa kuwanunua.