Zaburi 114
Maajabu Ya Mungu Wakati Israeli Walipotoka Misri 
 
1 Wakati Israeli walipotoka Misri,  
nyumba ya Yakobo kutoka kwa watu wa lugha ngeni,   
2 Yuda alifanywa makao matakatifu ya Mungu,  
Israeli akawa milki yake.   
   
 
3 Bahari ilitazama ikakimbia,  
Yordani ulirudi nyuma,   
4 milima ilirukaruka kama kondoo dume,  
vilima kama wana-kondoo.   
   
 
5 Ee bahari, ni nini kilichokufanya ukakimbia,  
nawe, ee Yordani, ukarudi nyuma,   
6 enyi milima mkarukaruka kama kondoo dume,  
enyi vilima, kama wana-kondoo?   
   
 
7 Ee dunia, tetemeka mbele za Bwana,  
mbele za Mungu wa Yakobo,   
8 aliyegeuza mwamba kuwa dimbwi la maji,  
mwamba mgumu kuwa chemchemi za maji.