Zaburi 101
Ahadi Ya Kuishi Kwa Uadilifu Na Kwa Haki 
 
Zaburi ya Daudi. 
 
1 Nitaimba juu ya upendo wako na haki yako;  
kwako wewe, Ee Bwana, nitaimba sifa.   
2 Nitazingatia kuishi maisha yasiyo na lawama:  
utakuja kwangu lini?  
   
 
Nitatembea nyumbani mwangu  
kwa moyo usio na lawama.   
3 Sitaweka mbele ya macho yangu  
kitu kiovu.  
   
 
Ninayachukia matendo ya watu wasio na imani;  
hawatashikamana nami.   
4 Moyo wa ukaidi utakuwa mbali nami;  
nitajitenga na kila ubaya.   
   
 
5 Kila amsingiziaye jirani yake kwa siri,  
huyo nitamnyamazisha;  
mwenye macho ya dharau na moyo wa kiburi  
huyo sitamvumilia.   
   
 
6 Macho yangu yatawaelekea waaminifu katika nchi,  
ili waweze kuishi pamoja nami;  
yeye ambaye moyo wake hauna lawama  
atanitumikia.   
   
 
7 Mdanganyifu hatakaa  
nyumbani mwangu,  
yeye asemaye kwa uongo  
hatasimama mbele yangu.   
   
 
8 Kila asubuhi nitawanyamazisha  
waovu wote katika nchi;  
nitamkatilia mbali kila mtenda mabaya  
kutoka mji wa Bwana.