4
Kujaribiwa Kwa Yesu
(Marko 1:12-13; Luka 4:1-13)
Kisha Yesu akaongozwa na Roho Mtakatifu kwenda nyikani ili akajaribiwe na ibilisi. Baada ya kufunga siku arobaini usiku na mchana, hatimaye akaona njaa. Mjaribu akamjia na kumwambia, “Ikiwa wewe ndiye Mwana wa Mungu, amuru mawe haya yawe mikate.”
Lakini Yesu akajibu, “Imeandikwa: ‘Mtu haishi kwa mkate tu, ila kwa kila neno litokalo katika kinywa cha Mungu.’ ”
Ndipo ibilisi akamchukua Yesu mpaka mji mtakatifu na kumweka juu ya mnara mrefu wa Hekalu, akamwambia, “Kama wewe ndiwe Mwana wa Mungu jitupe chini. Kwa kuwa imeandikwa:
“ ‘Atakuagizia malaika zake,
nao watakuchukua mikononi mwao
ili usije ukajikwaa mguu wako katika jiwe.’ ”
Yesu akamjibu, “Pia imeandikwa: ‘Usimjaribu Bwana Mungu wako.’ ”
Kwa mara nyingine, ibilisi akamchukua Yesu mpaka kwenye kilele cha mlima mrefu na kumwonyesha falme zote za dunia na fahari zake, kisha akamwambia, “Nitakupa hivi vyote kama ukinisujudia na kuniabudu.”
10 Yesu akamwambia, “Ondoka mbele yangu, Shetani! Kwa maana imeandikwa, ‘Mwabudu Bwana Mungu wako, na umtumikie yeye peke yake.’ ”
11 Ndipo ibilisi akamwacha, nao malaika wakaja na kumhudumia.
Yesu Aanza Kuhubiri
(Marko 1:14-15; Luka 4:14-15)
12 Yesu aliposikia kwamba Yohana Mbatizaji alikuwa ametiwa gerezani, alirudi Galilaya. 13 Akaondoka Nazareti akaenda kuishi Kapernaumu, mji ulioko karibu na bahari, katika mipaka ya nchi ya Zabuloni na Naftali, 14 ili kutimiza unabii wa nabii Isaya, kama alivyosema:
15 “Nchi ya Zabuloni na nchi ya Naftali,
kwenye njia ya kuelekea baharini,
ngʼambo ya Yordani,
Galilaya ya watu wa Mataifa:
16 watu wale waliokaa gizani
wameona nuru kuu;
nao wale walioishi katika nchi ya uvuli wa mauti,
nuru imewazukia.”
17 Tangu wakati huo, Yesu alianza kuhubiri akisema: “Tubuni, kwa maana Ufalme wa Mbinguni umekaribia.”
Yesu Awaita Wanafunzi Wake Wa Kwanza
(Marko 1:16-20; Luka 5:1-11)
18 Yesu alipokuwa anatembea kando ya Bahari ya Galilaya, aliwaona ndugu wawili, Simoni aitwaye Petro, na Andrea ndugu yake. Walikuwa wakizitupa nyavu zao baharini kwa kuwa wao walikuwa wavuvi. 19 Yesu akawaambia, “Njooni, nifuateni nami nitawafanya mwe wavuvi wa watu.” 20 Mara wakaziacha nyavu zao, wakamfuata.
21 Alipoendelea mbele kutoka pale, akawaona ndugu wengine wawili, Yakobo mwana wa Zebedayo na Yohana nduguye, wakiwa wamekaa kwenye mashua pamoja na baba yao Zebedayo, wakizitengeneza nyavu zao. Yesu akawaita. 22 Nao mara wakaiacha mashua yao, pamoja na baba yao, wakamfuata.
Yesu Ahubiri Na Kuponya Wagonjwa
(Luka 6:17-19)
23 Yesu akapita katika Galilaya yote, akifundisha katika masinagogi yao, akihubiri habari njema za Ufalme, na akiponya kila ugonjwa na kila aina ya maradhi miongoni mwa watu. 24 Kwa hiyo sifa zake zikaenea sehemu zote za Shamu, nao watu wakamletea wote waliokuwa na magonjwa mbalimbali na maumivu, waliopagawa na pepo wachafu, wenye kifafa na waliopooza, naye akawaponya. 25 Makutano makubwa ya watu yakawa yanamjia kutoka Galilaya, Dekapoli,* Yerusalemu, Uyahudi na kutoka ngʼambo ya Mto Yordani.
* 4:25 Yaani Miji Kumi.