46
Yakobo Aenda Misri
Hivyo Israeli akaondoka na vyote vilivyokuwa mali yake, naye alipofika Beer-Sheba, akamtolea dhabihu Mungu wa Isaki baba yake.
Mungu akanena na Israeli katika maono usiku na kusema, “Yakobo! Yakobo!”
Akajibu, “Mimi hapa.”
Mungu akamwambia, “Mimi ndimi Mungu wa baba yako, usiogope kushuka Misri, kwa maana huko nitakufanya taifa kubwa. Nitashuka Misri pamoja nawe, nami hakika nitakurudisha tena Kanaani. Mikono ya Yosefu mwenyewe ndiyo itakayofunga macho yako.”
Ndipo Yakobo akaondoka Beer-Sheba nao wana wa Israeli wakamchukua baba yao Yakobo na watoto wao na wake zao katika magari ya kukokotwa yale Farao aliyokuwa amempelekea kumsafirisha. Wakachukua pia mifugo yao na mali walizokuwa wamezipata Kanaani, Yakobo na uzao wake wote wakashuka Misri. Akawachukua wanawe na binti zake, wajukuu wake wa kiume na wa kike, yaani uzao wake wote mpaka Misri.
 
Haya ndiyo majina ya wana wa Israeli (Yakobo na wazao wake), waliokwenda Misri:
 
Reubeni mzaliwa wa kwanza wa Yakobo.
Wana wa Reubeni ni:
Hanoki, Palu, Hesroni na Karmi.
10 Wana wa Simeoni ni:
Yemueli, Yamini, Ohadi, Yakini, Sohari na Shauli mwana wa mwanamke Mkanaani.
11 Wana wa Lawi ni:
Gershoni, Kohathi na Merari.
12 Wana wa Yuda ni:
Eri, Onani, Shela, Peresi na Zera (lakini Eri na Onani walifariki katika nchi ya Kanaani).
Wana wa Peresi ni:
Hesroni na Hamuli.
13 Wana wa Isakari ni:
Tola, Puva, Yashubu na Shimroni.
14 Wana wa Zabuloni ni:
Seredi, Eloni na Yaleeli.
15 Hawa ndio wana wa Lea aliomzalia Yakobo huko Padan-Aramu pamoja na binti yake Dina. Jumla ya wanawe na binti zake walikuwa thelathini na watatu.
 
16 Wana wa Gadi ni:
Sefoni, Hagi, Shuni, Esboni, Eri, Arodi na Areli.
17 Wana wa Asheri ni:
Imna, Ishva, Ishvi na Beria.
Dada yao alikuwa Sera.
Wana wa Beria ni:
Heberi na Malkieli.
18 Hawa ndio watoto Zilpa aliomzalia Yakobo, ambao Labani alimpa binti yake Lea; jumla yao walikuwa kumi na sita.
 
19 Wana wa Raheli mke wa Yakobo ni:
Yosefu na Benyamini. 20 Huko Misri, Asenathi binti wa Potifera, aliyekuwa kuhani wa mji wa Oni,* alimzalia Yosefu wana wawili, Manase na Efraimu.
21 Wana wa Benyamini ni:
Bela, Bekeri, Ashbeli, Gera, Naamani, Ehi, Roshi, Mupimu, Hupimu na Ardi.
22 Hawa ndio wana wa Raheli aliomzalia Yakobo; jumla yao ni kumi na wanne.
 
23 Mwana wa Dani ni:
Hushimu.
24 Wana wa Naftali ni:
Yaseeli, Guni, Yeseri na Shilemu.
25 Hawa walikuwa wana wa Bilha aliomzalia Yakobo, ambaye Labani alikuwa amempa Raheli binti yake; jumla yao walikuwa saba.
 
26 Wote waliokwenda Misri pamoja na Yakobo, waliokuwa wazao wake hasa pasipo kuhesabu wakwe zake, walikuwa watu sitini na sita. 27 Pamoja na wana wawili waliozaliwa na Yosefu huko Misri, jumla yote ya jamaa ya Yakobo, waliokwenda Misri, walikuwa sabini.
 
28 Basi Yakobo akamtanguliza Yuda aende kwa Yosefu ili amwelekeze njia ya Gosheni. Walipofika nchi ya Gosheni, 29 gari kubwa zuri la Yosefu liliandaliwa, naye akaenda Gosheni kumlaki baba yake Israeli. Mara Yosefu alipofika mbele yake, alimkumbatia baba yake, akalia kwa muda mrefu.
30 Israeli akamwambia Yosefu, “Sasa niko tayari kufa, kwa kuwa nimejionea mwenyewe kwamba bado uko hai.”
31 Ndipo Yosefu akawaambia ndugu zake na watu wa nyumbani mwa baba yake, “Nitapanda kwa Farao na kumwambia, ‘Ndugu zangu na watu wa nyumbani mwa baba yangu, waliokuwa wakiishi katika nchi ya Kanaani, wamekuja kwangu. 32 Watu hao ni wachunga mifugo, huchunga mifugo, wamekuja na makundi ya kondoo, mbuzi na ngʼombe pamoja na kila kitu walicho nacho.’ 33 Farao atakapowaita na kuwaulizeni, ‘Kazi yenu ni nini?’ 34 Mjibuni, ‘Watumwa wako wamekuwa wachunga mifugo tangu ujana wetu mpaka sasa, kama baba zetu walivyofanya.’ Ndipo mtakaporuhusiwa kukaa katika nchi ya Gosheni, kwa kuwa wachunga mifugo wote ni chukizo kwa Wamisri.”
* 46:20 Yaani Heliopoli (Mji wa Jua).